DHAMIRA ya Serikali kununua ndege mpya
na kuimarisha Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) sasa ni dhahiri kutokana na Rais
John Magufuli jana kukutana na Mkurugenzi wa Masoko ya Afrika wa Kampuni ya
utengenezaji ndege ya Boeing.
Rais Magufuli alizungumza jana Ikulu,
Dar es Salaam na Jim Deboo wea kampuni hiyo yenye makao yake Marekani ikiwa ni
sehemu ya juhudi za Serikali za kununua ndege kubwa za kampuni hiyo.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, ilisema mazungumzo hayo yalihudhuriwa
na Katibu Mkuu Uchukuzi, Dk Leonard Chamriho na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha
na Mipango, Doto James.
Baada ya Mazungumzo hayo Rais Magufuli
alisema Serikali yake imedhamiria kununua ndege zingine nne zikiwamo kubwa tatu
ambazo zitasaidia kuinua uchumi wa nchi kwa kuwezesha watalii kuja nchini moja
kwa moja kwao.
"Sisi tunazungumza kuwa watalii
hawajafika hata milioni mbili kwa mwaka, lakini nchi ya Morocco inapata watalii
zaidi ya milioni 12 kwa mwaka, hii yote ni kwa sababu hatuna mashirika ya ndege
ya kwetu.
“Watalii wakitaka kuja hapa ni lazima
waje kwa kuungaunga, wafikie nchi nyingine ndipo wapate moyo wa kuja huku, licha
ya kwamba sisi ni miongoni mwa nchi tano duniani zenye maeneo mazuri yenye
utalii.
"Kwa hiyo niwaombe tu Watanzania
wapende mali zao, kwa sababu wakati mwingine nikiangalia mitandao na magazeti,
ni ajabu huwezi kuamini kama hao ni Watanzania, wanasifia tu ndege za watu
wengine na wanazibeza zao," alisisitiza
Rais Magufuli.
Rais alitaja aina ya ndege mpya ambazo
Serikali itanunua kuwa ni moja ya Bombardier Q400 Dash 8 NextGen inayotarajiwa kufika nchini Juni mwakani, mbili za
Bombardier CS300 zenye uwezo wa kubeba abiria kati ya 137 na 150 na
zinazotarajiwa kuwasili nchini kati ya Mei na Juni, 2018.
Pia ndege aina ya Boeing 787 Dash 8
Dream Liner yenye uwezo wa kubeba abiria 262 na inayotarajiwa kuwasili nchini
Juni, 2018. Malipo ya awali kwa ndege hizo yameshafanyika.
Dk Magufuli alitaka Watanzania kuunga
mkono juhudi hizo zenye lengo la kuinua utalii na kuimarisha uchumi wa nchi.
"Tumeleta ndege aina ya Bombardier,
zimepunguza gharama za safari, mfano kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza, sasa
wanalipa kati ya Sh 160,000 na Sh 200,000 wakati nauli ilishafika Sh. 800,000 na
kitu, lakini watu wengine wanazungumzazungumza wee maneno ya hovyo kwa
kutumiwa, tumeshaamua na tutafanya hivyo," alisisitiza Rais.
Wakati huo huo, Rais Magufuli aliagana
na aliyekuwa Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika nchini (AfDB) Dk
Tonia Kandiero ambaye amepanda cheo na kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AfDB) Ukanda wa Kusini mwa Afrika katika ofisi zake za
Afrika Kusini.
Rais Magufuli alimshukuru Dk Kandiero
kwa juhudi kubwa alizofanya nchini ambapo miradi mikubwa na muhimu katika
maendeleo imetekelezwa na inaendelea kutekelezwa.
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli aliagana
na Balozi wa Cuba nchini, Jorge Luis Lopez Tormo anayemaliza muda wake, baada
ya kuiwakilisha nchi yake kwa miaka minne.
Rais Magufuli alimshukuru Tormo kwa
ushirikiano mzuri aliouendeleza kati ya Tanzania na Cuba uliojengwa na waasisi
Baba wa Taifa marehemu Mwalimu Julius Nyerere wa Tanzania na Fidel Castro.
Tormo amemshukuru Rais Magufuli na
Serikali kwa kuendeleza ushirikiano mzuri wa Tanzania na Cuba na
kusema anaondoka akiamini kuwa uhusiano wa nchi hizi utaendelea kunufaisha
wananchi kupitia miradi mikubwa ya maendeleo na huduma za kijamii.
0 comments:
Post a Comment