Ajali 2 zaua 12 Iringa


Francis Godwin, Iringa

Ajali ya Iringa
JINAMIZI la ajali limeutikisa mkoa baada ya watu 12 kufa na wengine 31 kujeruhiwa kwenye ajali mbili tofauti ndani ya saa sita za usiku mmoja.

Hali hiyo ambayo imeacha simanzi kubwa kwa wananchi wa hapa na mikoa jirani ya Njombe na Mbeya, usiku wa kuamkia jana ililiza wananchi wa Tanangozi, Kalenga kutokana na wananchi wake tisa kufa papo hapo huku 18 wakijeruhiwa.

Hiyo ilitokana na ajali iliyotokea saa 11.45 jioni juzi baada ya lori namba T 970 AJT lililokuwa likiendeshwa na Francis Peter kutoka Mbeya kuja mjini hapa kugonga gari dogo aina ya Toyota Hiace namba T 920 DBA lililokuwa likiendeshwa na Sebastian Njau.

Wananchi wa hapa hususan wa Ulete ambako Hiace ilikuwa ikienmda wakiwa na wakati mgumu wa kutaka kujua majina ya ndugu waliopoteza maisha kwenye ajali hiyo hadi saa 4 usiku walikuwa eneo la ajali Tanangozi.

Hapo walikuwa na viongozi mbali mbali wa Polisi na Serikali chini ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza ambapo pia saa 5 usiku ajali nyingine ikatokea kwa basi la Ngasamo Express lililokuwa likitoka Mwanza kwenda Mbeya lilipopinduka Mafinga.

Mashuhuda wa tukio hilo waliozungumza na mwandishi wa habari hizi wakiwa eneo la tukio Tanangozi, walidai kuwa Hiace ni mali ya Kastoli Maluli na ilisimama kushusha abiria na wakati ikiondoka ndipo lori hilo lililofeli breki likaipamia.

John Kalinga alisema kutokana na lori kuwa kwenye mwendo kasi, nusu ya abiria waliokuwa kulia walipoteza maisha huku baadhi ya miili ikinyofoka mikono na miguu na kukutwa kwenye lori umbali wa zaidi ya meta 15 kutoka ilipokuwa Hiace.

Hata hivyo, shuhuda huyo alisema miili mingi ni ya wanaume na kwamba madereva wa magari yote walinusurika na kukimbizwa kwenye hospitali ya Rufaa ya Mkoa.

Inasemekana baadhi ya majeruhi na waliopoteza maisha kwenye ajali hiyo walikuwa ni waenda kwa miguu.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Julius Mjengi alithibitisha kutokea kwa ajali hizo.

Alisema basi lililopinduka lilikuwa likiendeshwa na Amos Yoyo na kuwa majeruhi wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mufindi mjini Mafinga na miili ya marehemu imehifadhiwa kwenye mochari ya hospitali hiyo.

Kutokana na ajali hizo, Masenza aliiagiza Polisi kuanzisha ukaguzi wa magari yote na kuchukua hatua kali.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Iringa, Julius Mjengi (wa pili kulia) akitazama mabaki ya Toyota iliyogongwa na lori eneo la Tanangozi, Iringa, juzi usiku. (picha na Francis Godwin).
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo