ACT-Wazalendo yamshauri JPM kuhusu ATCL


Leonce Zimbandu

Zitto Kabwe
CHAMA cha ACT-Wazalendo kimemshauri Rais John Magufuli kuunda kitengo cha huduma za chini za uendeshaji wa viwanja vya ndege, badala ya kuvibinafsisha.

Huduma hizo ni utunzaji wa mizigo, abiria, mfumo wa kompyuta, usafirishaji na upokeaji mizigo na usafiri wa mabasi kutoka na kwenda uwanja wa ndege.

Zingine ni mfumo wa usalama wa viwanja, kitengo cha uhandisi cha kukarabati ndege zinazoharibika na huduma ya kuuza mafuta isiwe lazima zipewe kampuni za Puma au Oilcom.

Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Anna Mghwira alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana.

Alisema lengo la kuboresha sekta ya anga iwe ni kurudishia Shirika la Ndege la Taifa (ACTL) mamlaka ya kumiliki huduma zote za chini za uendeshaji wa viwanja vya ndege.

“Ni vema huduma za chini zikaimarishwa haraka, kabla ndege zingine nne kuwasili nchini, kwa vile huduma hizo ni vitega uchumi vya mashirika  yote ya ndege duniani, ACTL itapata fedha nyingi ikisimamia huduma hizo,” alisema.

Alisema anashangaa Tanzania kwenda kinyume na utaratibu unaotumiwa na mataifa mengine ambayo viwanja vya ndege vinamilikiwa na wananchi Wazalendo.

Aliongeza kuwa utaratibu wa kimataifa unataka mamlaka ya usimamizi wa viwanja vya ndege umilikiwe na Wazalendo walioajiriwa kwenye mamlaka hiyo, ili kulinda usalama wa viongozi.

Aidha, Mghwira alisema udhaifu wa viwanja vya ndege ulianza mwaka 1990 baada ya viongozi kujihusisha na ufisadi wa kuuza mali za umma kwa wageni bila kujali usalama wa nchi.

Alisema mashirika matano hayakupaswa kubinafsishwa, likiwamo ATC, Wakala wa Meli Tanzania (NASACO) na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).

Mengine ni Benki ya Taifa ya  Biashara (NBC) na Shirika la Simu Tanzania (TTCL), ubinafsishaji huo ulifanyika kwa kuzingatia rushwa ya asilimia 10, kwamba hiyo ni aibu ya kudumu Tanzania.

Katika kipindi hicho, alisema shirika hilo lilianza kuyumba baada viongozi wa Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi, Idara ya Anga kuuza njia za ndege kwa mashirika mengine na kuingia mikataba mibovu.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo